Katavi yakabiliwa na malaria
Mkoa wa Katavi umetajwa kukabiliwa na tatizo la malaria kwa asilimia 7 ambapo serikali kupitia Wizara ya Afya imeanza kugawa vyandarua 57,794 bure kwa kaya 156,859.
Mratibu wa Malaria Mkoa wa Katavi, Daktari Ramadhani Karume katika maadhimisho ya miaka 60 ya uhuru yaliyofanyika leo Desemba 08,2021 amesema watu 1,064,793 wameandikishwa.
Ametaja mikakati waliyonayo kupambana na tatizo hilo ni pamoja na kaya kuzigawia vyandarua hivyo kwa mgawanyo wa chandarua kimoja kwa matumizi ya watu wawili.
“Kuimarisha ufuatiliaji na tathmini ya malaria,kuhakikisha ifikapo 2025 maambukizi yanakuwa chini ya asilimia 3.5 na 2030 tutokomeze kabisa,”amesema Karume akaongeza
“Tutahakikisha tunatoa elimu ya uhamasishaji jamii juu ya matumizi sahihi ya vyandarua na kuondoa mila potofu kwamba vitaenedelea kutolewa kila siku,”
Ameongeza kuwa watahakikisha upatikanaji wa dawa na vitendanishi katika vituo vya kutolea huduma za afya unaimarishwa ,kujenga zahanati kila kijiji na kituo cha afya kila kata.
Naye Mkuu wa Mkoa wa Katavi Mwanamvua Mrindoko mara baada ya kuzindua ugawaji wa vyandarua hivyo amewataka wananchi wavitumie inavyokusudiwa.
“Wananchi vyandarua hivi ni kwaajili ya kujikinga na ugonjwa wa malaria na siyo kwenda kufugia vifaranga vya kuku,kutumia kwenye bustani za mchicha na matembele,”amesema Mrindoko akaongeza.
“Wala siyo vya kuweka uvunguni au juu ya dari, vimegharamiwa na serikali kwakushirikiana na wadau lengo lake ni kupunguza maambukizo ya malaria,”
Mmoja wakazi mkoani Katavi Ally Kamwelwe aliyepata vyandarua vinne kwaajili ya familia yake ameishukuru serikali kutoa msaada huo akidai kuwa ni mkombozi kwa walio na maisha duni.
“Tulikuwa tunalala chandarua kwasababu sikuwa na uwezo wa kununua,vitatusaidia kujikinga na malaria,”amesema Kamwelwe.
Comments
Post a Comment