Johnson asifu makubaliano yaliyofikiwa COP26
Waziri Mkuu wa Uingereza Boris Johnson ameyasifu makubaliano yaliyofikiwa wakati wa mkutano wa kimataifa wa mabadiliko ya tabianchi uliomalizika mjini Glasgow akisema yanafungua njia ya "mageuzi makubwa" licha vizingiti vichache vilivyosalia.
Johnson amesema moja ya mafanikio makubwa ya mkataba uliopatikana ni shinikizo kwa ulimwengu kuachana na matumizi ya nishati ya makaa ya mawe inayohusishwa na uchafuzi mkubwa wa mazingira.
Waziri huyo mkuu wa Uingereza ambaye alikuwa mwenyeji wa mkutano huo huko Scotland amesema ahadi ya bara la Ulaya na Marekani ya kuondoa ufadhili kwenye miradi ya makaa ya mawe na mafuta mazito ni hatua muhimu kuelekea usitishaji matumizi ya nishati chafuzi.
Hata hivyo licha ya mafanikio aliyoyataja, Johnson amekiri kuwa mkutano huo wa COP26 haukutoa suluhisho kamili la kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi duniani.
Comments
Post a Comment